Rais KIkwete akizungumza na viongozi wa Serikali.
Kwa mshangao mkubwa, tunashuhudia maofisa wa Serikali wakiendelea kutoa kauli zinazokinzana kila kukicha.
Haijapata kutokea tangu nchi yetu ipate uhuru
watendaji wakuu serikalini kutoa kauli zinazopishana na kukinzana, tena
katika masuala mazito ya kitaifa yanayohusu mustakabali wa nchi yetu.
Inavyoonekana sasa ni kuwa, pengine mkanganyiko
uliomo ndani ya Serikali ya Awamu ya Nne ni matokeo ya kukosekana kwa
uongozi wa pamoja.
Tunazungumzia hapa kauli zinazotolewa na baadhi ya
viongozi waandamizi serikalini kuhusu masuala mbalimbali ya kitaifa,
ikiwa ni pamoja na tarehe ya kufanyika Kura ya Maoni kuhusu ‘Katiba
Inayopendekezwa’,
Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na uboreshwaji wa
Daftari la Kudumu la Wapigakura. Inasikitisha kuona ndani ya Serikali
kila mmoja anasema lake kama vile hakuna utaratibu wa kufanya uamuzi wa
pamoja kuhusu masuala hayo.
Kwa mfano, kauli iliyotolewa juzi na Mwanasheria
Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema kwamba Kura ya Maoni
itafanyika Machi 30 mwakani na kwamba upigaji kura utatanguliwa na
kampeni ambazo zitafanyika kwa siku 30 kuanzia mwanzoni mwa Machi
imewashtua watu wengi.
Tunasema hivyo kwa kuwa ameitoa wakati akijua
kwamba tayari mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Damian
Lubuva ametangaza kwamba Tume yake haitaendesha uchaguzi wa aina
yoyote, ukiwamo wa Kura ya Maoni hadi uboreshaji wa Daftari la
Wapigakura utakapokuwa umekamilika.
Jaji Lubuva alisema wiki mbili zilizopita kwamba
kuendesha chaguzi bila kwanza kuboresha Daftari hilo ni kuongeza
malalamiko kutoka kwa wananchi na wadau wengine, vikiwamo vyama vya
siasa.
Mkanganyiko unaotokana na misimamo hiyo ya AG na
kiongozi wa NEC ni kwamba viongozi hao wanakubaliana kwamba Kura ya
Maoni ifanyike baada ya Daftari hilo kuboreshwa. Maswali yanayojitokeza
ni kuwa, kama AG anatambua hilo, inakuwaje apange kwamba tarehe ya
kufanyika kwa kura hiyo ya maoni ni Machi 30 mwakani, huku akijua
msimamo wa NEC ni kwamba uboreshaji wa Daftari hilo hautakamilika hadi
Mei mwakani?
Inakuwaje aseme kampeni zitafanyika kuanzia
mwanzoni mwa Machi, huku akijua Sheria ya Mabadiliko ya Katiba inataka
muda huo itolewe elimu ya uraia kati ya miezi mitatu hadi sita kabla ya
kufanyika kwa kura hiyo ya maoni?
Sheria hiyo imetoa jukumu hilo la utoaji wa elimu
hiyo kwa NEC, hivyo AG anapozungumzia kampeni wakati huo anazidi
kuwapotosha na kuwachanganya wananchi. Hiyo inatukumbusha kauli ya
Waziri Mkuu katika Bunge la Katiba kwamba Kura ya Maoni ifanyike kabla
ya Uchaguzi Mkuu wa 2015, huku Rais Jakaya Kikwete akisema ifanyike
baada ya uchaguzi huo ili kutoa nafasi ya uboreshaji wa Daftari la
Wapigakura.
Wakati huohuo, Rais Kikwete alisema hivi karibuni
kwamba Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ufanyike Februari mwakani, lakini
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akatangaza baadaye kwamba uchaguzi huo
utafanyika Desemba mwaka huu.
Lakini wakati mambo hayajawekwa sawa, jana Rais Kikwete akiwa
ziarani nchini China, alitangaza kwamba Kura ya Maoni itafanyika Aprili
mwakani.
Kauli hizo zimezidi kuwachanganya wananchi. Sisi
tunasema unahitajika uongozi wa pamoja ndani ya Serikali. Nchi inapokuwa
na viongozi ambao kila mmoja anatoa kauli inayokinzana na ya mwenzake,
matokeo yake ni mfarakano ambao hakika hauwezi kuleta umoja na
mshikamano katika kusimamia sheria za nchi na kuwaletea wananchi
maendeleo.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment